Wednesday, 5 March 2014

MAKALA: KAMA HUJAFELI BASI HUJAJARIBU, NA USIPOJARIBU HUWEZI KUFANIKIWA


Mgunduzi wa taa, Thomas Edison alijaribu zaidi ya mara 1000 hadi akafanikiwa.
                          Kwa maisha ya hivi sasa, ni habari ya kuchakarika kwa kwenda mbele. Sizungumzii wale wanaojipatia mali kwa njia iliyopinda, mathalani utapeli, wizi, na hata ujambazi wa kalamu na mwili, la hasha. Nazungumzia kuchakarika kwa mtu kudamkia kazi mapema iwezikanavyo, kabla hata ya wengine hawajamaliza ndoto zao.

Nikiwa mjini Dodoma, nakutana na mzee Hamisi, yeye ni dereva wa taksi, na nilipomuuliza hii kazi anaifanya tokea lini, ndipo akaniambia kuwa tokea mwaka 1996. Yaani hadi hivi sasa ni kipindi cha miaka 18, na akaongeza kuwa anaendesha maisha kwa mfumo huo hadi sasa, yaani kulipia ada za watoto, kujenga nyumba na hata mahitaji ya kila siku sasa, wanakula na kwenda chooni kama kawaida.

Hapo ndipo nikambukuka kijana mmoja ambaye nilikutana naye mitaa ya Posta jijini Dar es Salaam, ambaye yeye biashara yake ni kuuza madafu. Kama kawaida mpenda madafu mie nikapiga breki ya miguu na kujipatia mawili (nimeyakosa kwa muda mrefu aisee). Katika stori za hapa na pale, akaeleza kuwa anatumia masaa 4 kwenda na kurudi kwa baiskeli hadi kuyafikisha mjini. Na siku hiyo, anasema kwamba hakuwa na mengi, ila madafu 69 tu, ambayo alianza kuuza mida ya saa saba mchana na kufikia saa tisa hakuwa na kitu. Nikajifunza jambo, nikashukuru na kuishia.

Na kwa sasa namkumbuka kijana mmoja mjini Same ambaye ni fundi viatu. Yeye ni habari ya kushona na kung'arisha, benchi lake kaliweka kando ya ukuta na hana maneno na mtu, anasubiria mtu aje – mwenye haja na kurekebisha lapa au kiatu, chochote kinachovaliwa mguuni ambacho kitaleta mushkeli, basi yeye yupo kurekebisha. Na yeye sikuacha kumuuliza mawili matatu, naye akanieleza kuwa kabla ya kuanza siku, ni lazima aikabidhi mikononi mwa BWANA, ili mambo yaende sawa – na kwa maelezo yake, hajawahi kuangushwa na BWANA Mungu.

Sasa nirudi kwenye mada husika, mara nyingi vijana mtaani na hata mjini wanaogopa kufanya jambo fulani kwa maelezo kuwa ni jambo hilo ni gumu. Yaani kwamba hata wakifanya watafeli, na hivyo kurudi nyuma, kwamba kuliko kufeli ni afadhali ya kutofanya kabisa. Ndio hai vijana wapo, huenda hata wewe umeshafikiria kufanya jambo fulani ukaogopa kufeli, na hivyo ukaachana nalo.

Sasa basi nikukumbushe, kwa wale ambao walibahatika kufika sekondari, wakati unamaliza darasa la saba, nina hakika wengi waliambiwa kuwa kidato cha kwanza ni kigumu na sio sehemu ya kufanya mchezo, huenda wengine waliacha shule kwa kusikia hivyo, siok hata kujaribu, ila tu kwa kusikia. Na wewe uliyefanikiwa kujitosa kuendelea, aidha klwa kulazimishwa ama kwa shauku ya kujua ugumu wake ni nini, ama tu kwa vile ulishaelezwa kuwa elimu ni ufunguo wa maisha, hakika ulifika na ukasoma kama kawaida, licha ya kuhofia masomo ya kiingereza, sijui bunsen burner, mara sijui litmus paper, ama bank reconciliation account, yote hayo uliyakuta na kuvuka, na hatimaye kufika kidato cha tano na cha sita, huko nako ni habari nyingine.

Lakini kwa huu mfano wa kuvuka darasa la saba, ni dhahiri kwamba kma usingejaribu basi na usingefanikiwa. Hata kufikia kidato cha nne, wengine hawakufanya mtihani, ila waliofanya aidha walifeli ama kufaulu. Waliofaulu wakasonga mbele, na waliofeli wakarudi kutafakari chanzo cha kuanguka na kisha kujipanga upya kwa ajili ya kufanya mtihani wa taifa kwa mara nyingine.

Sasa basi, ni dhahiri kuwa ujinga tulionao ndio unaotufanya tusisonge mbele kwenye mipango na mikakati tuliyonayo maishani. Kwa mfano, unaogopa kuanza kozi unayotaka chuoni kwa kuwa huamini kama utafanikiwa kuvuka.. ama unaogopa kuulizia hata bei ya kiwanja kwa sababu unaamini huna hata hela,a achilia mbali pesa.. pengine unaopoga kumuambia kuwa unampenda, ilhali anasubiria.. huenda unashindwa kuendelea kiuchumi kwa kuwa unaogopa kuweka genge la matunda hapo nje.. ati matunda ni ya msimu, kwa hiyo watu hawatakuja sana..


Kama Mzee Hamisi angeangalia idadi ya taksi zilizopo barabarani, basi asingeingia kwenye biashara hizo, kama huyu kijana muuza madafu angeangalia jasho litakalomtoka kwenda na kurudi kila siku kufuata madafu hayo, basi angeachana na habari ya shughuli hiyo kabisa, na labda tu nikuambie ameshakamatwa na mgambo wa jiji kama leo, ila kesho akarudi palepale, amethubutu hadi wakaelewa kuwa “huyu pia ni msakatonge, tuachane nae”. Na kama fundi viatu angesema duka analoshabihiana nalo ni kubwa na lina viatu vipya tu vilivyo bora, basi asingefungua eneo lake hilo.

Na wewe ukiangalia bodaboda zilivyo nyingi barabarani ukasema usinunue kwamba haitakulipa, hiyo ni shauri lako mwenyewe, ambalo niko kinyume nalo, ama ukisema kuna 'bajaj' nyingi sana mjini na zinatosha kwa shughuli ya usafirishaji - kwamba labda utafute kitu kingine, hayo ni mawazo yako mwenyewe, na huna hata haja ya kumtafuta mchawi hapo.

Si unakumbuka, Lolote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako... kwenye Mhubiri 9:10 imeandikwa.

Sasa kama tatizo lako ni kusubiria 'memo' kutoka kwa Bwana mkubwa fulani ili mambon yako yaende sawa, basi unaweza ukawa umejichangana vizuri sana. Unamtegemea nani katika mambo yako? Wenzio wanarejea NENO, ya kwamba Msaada wangu u katika BWANA aliyezifanya mbingu na nchi. Zaburi 121 imeandikwa.

Kama unaamini cheti chako kiko vizuri, lakini kila ukitoka nacho kinarudi kama vile hakijapitiwa huko ulikokipeleka, basi ujue huu ndio muda mzuri wa kumuambia Mungu, kwanini mambo yako tu yaende kombo? Mwanzo mzuri ni kwa kuomba rehema, kutubu na kumtanguliza yeye katika mambo yetu yote.

Hata unapotoka, ni watu wengi unakutana nao, wengine wenye mpango wa kukuangusha ili mradi tu, na wengine hata sio watu kabisa, wanaonekana tu wanatembea, kumbe wako katika ulimwengu tofauti kabisa.

Yafuatayo ni muhimu, kabla ya kutoka uikabidhi siku kwa BWANA Yesu;

Ukitoka uwe umeomba kibali kwake Yesu, maana akikukubali yeye, mwanadamu ni nani apinge? Esta alipopata kibali kwa mfalme, hakuna aliyeweza kumpinga wala kumfanya 'apotezewe', kila kitu kiliuwa sawa hata kupelekea kuokolewa kwa kizazi cha Israel, huku mtesi wao, Hamani, akiipata fresh Esta 7

Ni muhimu pia ukaomba mwongozo wake, kupitia Luka 21:15, amesema atakupa kinywa na hekima ambayo watesi wako wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga. Sawa sawia wale wote ambao unaona ni kikwazo kwenye ofisi unayopeleka application yako, hebu omba kinywa na hekima - utapita katikati yao.

Kwa machache haya (yanaweza kuwa mengi pia), chukua hatua na ufanye jambo ambalo limekuwa likikutatiza, maana hauwezi ukaandika ripoti kama hujafanya chochote, vivyo hivyo huwezi kuelezea changamoto kama hujazipitia, jaribu sasa na ujue unatakiwa kufanya nini baada ya kufeli mara ya kwanza. Ukianguka, sharti usimame na kuendelea na safari tena - kama ambavyo mdunguzi wa balbu, mwanasayansi Thomas Edison alivyojaribu zaidi ya mara 1,000 hadi ikaja kuwaka, na alipoulizwa na mwandishi wa habari kwamba anajisikiaje kufeli mara elfu moja? Alijibu kuwa hajafeli, bali ugunduzi huo umepitia hatua tofauti 1,000. Wewe umepitia hatua ngapi hadi uchoke?

BWANA Yesu na akuwezeshe.

No comments:

Post a Comment